MGOMBEA urais wa Tanzania kwa tiketi ya CCM, Dk John Magufuli, jana
aliuteka mji wa Moshi mkoa wa Kilimanjaro, baada ya kuvuta umati mkubwa
wa watu aliowakuna kwa hotuba yake iliyosheheni ahadi nzito, zikiwamo za
kuondoa kero zinazowakabili na pia kuahidi kupaisha uchumi wa mkoa kwa
ujumla.
Katika mkutano wake wa kampeni mjini hapa, Magufuli alisema endapo
atachaguliwa kuwa Rais wa Awamu ya Tano baadaye mwezi huu, atahakikisha
Moshi inapaa kiuchumi. Ameahidi atashughulikia ukubwa wa ushuru,
kutolipwa vizuri kwa wabeba mizigo katika Mlima Kilimanjaro, kushuka kwa
utalii na kusema ana `dawa’ ya kuongeza idadi ya watalii kufikia
milioni mbili mjini Moshi.
Katika hotuba yake iliyokatishwa mara kwa mara kwa makofi, nderemo,
hoihoi na vifijo kutoka kwa wakazi wa mji huo, ambao kwa zaidi ya muongo
mmoja unaongozwa na chama cha upinzani cha Chadema, alitaka sasa
wakipumzishe chama hicho kwa kuwa kimeonekana kushindwa kuwapa wanaMoshi
maendeleo. Mbali ya kupania kupaisha utalii, alisema atarudisha viwanda
katika mji huo, huku akiwatengenezea wafanyabiashara mazingira bora ya
kufanya shughuli zao.
Alisema endapo atakuwa Rais, atahakikisha wafanyabiashara wa soko la
mitumba la Memorial hawahamishwi. “Bado siku 17, kwa kuwa wingi wenu
unaonesha mtanipa urais, niwahakikishie mtarajie mambo mazuri kutoka
Serikali ya Magufuli,” alisema na kusisitiza kama kuna mnunuzi
anayeshindwa kufufua kiwanda, ajiandae kupokonywa kwani huyo anakwamisha
ajira na maendeleo ya wakazi wa mkoa huo.
Alitumia pia fursa hiyo kumnadi mgombea ubunge wa CCM katika Jimbo la
Moshi, Davis Mosha akisema ni kijana mchapakazi na mwenye kiu ya kuweka
historia ya kuwapelekea wakazi wa Moshi maendeleo endelevu.
Awali, akiwa Bomang’ombe wilayani Hai, Dk Magufuli alisema pamoja na
urafiki wake na Mbowe, lakini uwezo wake katika kuwaletea maendeleo
wakazi wa Hai akiwa Mbunge ni mdogo na kuwataka wakazi wa jimbo hilo
kumchagua mgombea ubunge wa CCM, Dunstan Mallya.
Alisema pamoja na Halmashauri ya Wilaya ya Hai kuwa chini ya Chadema,
kero za wananchi ikiwemo maji, barabara na nyinginezo haziridhishi na
badala yake Mbowe amekuwa akisafiri Ulaya, kuzungukazunguka katika
majimbo mengine na kushabikia mambo yasiyo na msingi kwa wakazi wa Jimbo
la Hai.
Alishangazwa na hatua ya kutofanya kazi kwa Kiwanda cha Kilimanjaro
Machine Tools kilichopo wilayani Hai na kuua ajira kwa wakazi hao, huku
Mbowe akiwa kimya bila kuwasemea wananchi juu ya kitendo hicho hatua
aliyosema inatia shaka uhusiano wake na mmiliki wa kiwanda hicho wa
sasa.
Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM, Dk Emmanuel Nchimbi amesema Dk Magufuli
ni chaguo la Mungu. Alisema hilo linadhihirishwa na hatua ya mgombea
huyo, kutotumia fedha katika harakati zake za kuwania kuteuliwa na chama
hicho kuwa mgombea urais, lakini pia kwa wananchi kumuunga mkono kwa
nguvu tangu alipoanza kampeni za urais.
Aidha, Dk Nchimbi alieleza pia kukerwa na uzushi kwamba yupo mbioni
kujiunga na Umoja wa vyama vya upinzani vinavyounda Ukawa na kusema
uzushi huo ni ndoto ya mchana na kamwe hawezi kufanya hivyo kutokana na
upinzani kuwa katika hatua za kufa.
“Mimi kuhamia Ukawa ni ndoto ya mchana, haiwezekani mtu akashuka
kwenye basi la luxury (starehe) akahamia kwenye basi bovu ambalo
halijatembea kwa miaka zaidi ya 10. Upinzani umeelemewa na huu uzushi
kwangu unanikera na utawasababishia kipigo kikali Oktoba 25,” alisema.
Dk Magufuli na Dk Nchimbi waliyasema hayo kwa wakati tofauti kwenye
mikutano ya hadhara, iliyofanyika kwa siku nzima jana na kuhitimishwa na
mkutano mkubwa wa hadhara uliofanyika katika Dk John Magufuli uwanja wa
Mashujaa mjini Moshi.
Chanzo: Habarileo
Sign up here with your email