MIHURI YA 2010 YATUMIKA KUMAKI KARATASI ZA KURA
Upigaji kura katika baadhi ya vituo Manispaa ya Morogoro umeingia
dosari kutokana na baadhi waandikishaji kulazimika kutumia mihuri ya
mwaka 2010 baada ya ile ya sasa kugoma hali iliyozua malalamiko miongoni
mwa wagombea ubunge.
Akizungumzia tatizo hilo la mihuri, mgombea ubunge kupitia Chama
cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Jimbo la Morogoro Mjini ambacho
kinaungwa mkono na Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), Marcossy
Albaniel, alisema upigaji kura ulimekwenda vibaya kutokana na kutumika
kwa mihuli ya chaguzi zilizopita bila wao (wagombea) kushirikishwa.
Alizitaja baadhi ya kata zilizokumbwa na tatizo hilo la mihuri kuwa
ni vya kata za Mazimbu na Kihonda hali iliyopelekea kuchelewa kuanza
kwa upigaji wa kura.
Albaniel alisema baada ya kutokea kwa hali hiyo waliwasiliana na
Mkurugenzi wa Manispaa ya Morogoro ambaye ndiye msimamizi wa uchaguzi
lakini alishindwa kutoa majibu na badala yake kuamua kutumia mihuri hiyo
bila kuwashirikisha wagombea wala viongozi wa vyama.
“Tumejaribu kumpigia simu msimamizi wa uchaguzi wa manispaa lakini
simu zetu hapokei, kwakuwa amebadilisha utaratibu bila kutushirikisha na
sisi tunasema hatutaki mihuri hiyo iendelee kutumika,” alisema
Albaniel.
Mbali na hilo mgombea huyo alidai Jeshi la Polisi lilikuwa
likiwakataza wagombea kuingia katika vituo vya kupigia kura kuangalia
jinsi shughuli hiyo ilivyokuwa ikiendelea kinyume na utaratibu uliowekwa
na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec).
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chadema Wilaya ya Morogoro, James
Mkude, alisema ameshangazwa na msimamizi huyo wa uchaguzi kujichukulia
uamuzi wa kubadilisha mihuri bila kuwashirikisha wao kama viongozi wa
chama kilichosimamisha wagombea.
Naye mgombea ubunge katika jimbo hilo kupitia Chama cha Wakulima
(AFP), Mark Isdory, alisema hawakubaliani na kitendo kilichofanywa na
msimamizi wa uchaguzi wa Manispaa ya Morogoro kubadilisha mihuri ya
kupigia kura bila kuwashirikisha na kwamba wanahisi kuna vitendo vya
hujuma.
Chanzo: IPP media.
Sign up here with your email