Kada wa CCM Moshi Vijijini nusura auawe

Kada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Jimbo la Moshi Vijijini aliyefahamika kwa jina moja la Kizito, amenusurika kuuawa na wananchi wenye hasira katika kijiji cha Uru Mawela, baada ya kukamatwa akiwa na makaratasi yenye kura za mfano za wagombea wa ubunge na udiwani wa jimbo hilo.
Kizito aliyekuwa akitumia gari dogo aina ya Toyota Verosa lenye namba za usajili T 756 CPB, alikumbwa na mkasa huo jana saa 10:00 jioni wakati akitokea katika kituo cha kupigia kura cha Uru-Mawela. Katika tukio hilo, wananchi hao wanadaiwa kumjeruhi vibaya kada huyo na kisha kuliharibu gari lake kwa kuiba matairi yote manne, vifaa mbalimbali ikiwamo pia kadi ya usajili wa gari hilo.
Inadaiwa kuwa wananchi wa kijiji cha Uru-Mawela walimtilia shaka kada huyo na kuanza kumfuatilia tangu majira ya mchana na ilipofika saa 10 kasoro za jioni, walimvamia akiwa barabarani na kulifanyia upekuzi ambapo walimkuta akiwa na bahasha mbili zenye karatasi hizo ambazo hata hivyo, zilielezwa kuwa siyo karatasi halisi za kupigia kura.
Paparazi ilishuhudia kada huyo akiwa chini ya ulinzi wa magari mawili ya askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) waliowahi kufika eneo hilo na kumuokoa asiendelee kushambuliwa na wananchi hao na gari lake lisiteketezwe kwa moto.
Kamanda wa Polisi mkoani Kilimanjaro, Fulgence Ngonyani, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kueleza kwamba kada huyo baada ya kuokolewa alipelekwa Kituo Kikuu cha Polisi Moshi Mjini kwa ajili ya mahojiano kuhusiana na tukio hilo.
“Wananchi hao wenye hasira kali, wameliharibu vibaya gari la kada huyo na kuiba matairi yote, vifaa mbalimbali na kisha kulitelekeza likiwa limechakaa. Hata hivyo, huyo kada wa CCM tumemchukua na kumpeleka Kituo Kikuu cha Polisi Moshi Mjini kwa ajili ya kumhoji na baadaye tuanze operesheni za kuwasaka waliohusika katika tukio hilo,” alisema Kamanda Ngonyani.
Mgombea ubunge wa jimbo hilo kwa tiketi ya CCM, Dk. Cyril Chami, anachuana vikali na mpinzani wake wa siku nyingi Anthony Komu, ambaye pia ni Mkurugenzi wa Fedha na Utawala wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) taifa.
Previous
Next Post »
Show Comments: OR

Contact us

Name

Email *

Message *

Tangaza nasi

Tangaza nasi
Freebango.com