Mkanganyiko kukamatwa vifaa vya kupigia Kura


WAKAZI wa kata za Makuyuni na Kilema Kati wilayani Moshi Vijijini wamekamata baadhi ya masanduku na vifaa vya kupigia kura katika Jimbo la Vunjo juzi vinavyodaiwa kuwa ni kwa ajili ya kusaidia ushindi kwa baadhi ya wagombea.


Hata hivyo, baadaye ilielezwa kwamba vifaa hivyo ni halali. wakihojiwa Julius Materu na Alex Franklin walisema vifaa hivyo kukutwa mitaani katika kata hizo usiku ni maandalizi ya vyama kupata ushindi wa batili.

“Haiwezekani vifaa vya kura visafirishwe usiku tena bila ulinzi wa Polisi. Tunataka jambo hili lichunguzwe kikamilifu,” alisema Materu. Kwa upande wake, Kamanda wa Polisi mkoa wa Kilimanjaro, Fulgence Ngonyani alithibitisha kukamatwa kwa masanduku na vifaa vingine vya kupiga kura katika kata za Makuyuni na Kilema Kati na kwamba hapakuwa na ulinzi wa Polisi jambo ambalo pia limelitia shaka jeshi lake.

Alisema watu waliokamatwa na vifaa hivyo ni watumishi wa halmashauri na kwamba walikamatwa saa 4.15 usiku, hali iliyozua taharuki kiasi cha wananchi kuzunguka Kituo cha Polisi Himo.

“Ni kweli walikamatwa watu wawili wakiwa na vifaa vya kupigia kura, hata sisi tuliingiwa na wasiwasi kwamba kwanini hawakuwa na ulinzi wa Polisi, lakini tulipowahoji walidai ni watumishi wa halmashauri ndipo ilipoamuliwa vifaa vile vihifadhiwe Kituo cha Polisi Himo kwa usalama zaidi,” alisema.

Ngonyani alisema baada ya hali hiyo kutokea, Polisi ilimtaka Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Moshi, Fulgence Mponji ambaye aliwatambua watumishi hao na kusema kwamba vifaa hivyo ni halali na siyo vinginevyo.

Hata hivyo, vifaa hivyo vilisambazwa jana asubuhi kwa ajili ya kupigia kura ingawa Jeshi la Polisi kupitia maofisa wake wakiwamo wa mkoa wanafanya uchunguzi wa kina kuhusu tukio hilo na hasa ni kwa nini polisi hawakuwepo kwenye gari lililokuwa na vifaa hivyo.
Previous
Next Post »
Show Comments: OR

Contact us

Name

Email *

Message *

Tangaza nasi

Tangaza nasi
Freebango.com