TFF yamtaka Mkwasa kusuka, kunyoa


SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF) limemtaka kocha wa muda wa timu ya taifa Taifa Stars Charles Mkwasa kufanya maamuzi kama atabaki kuwa kwenye timu hiyo ama Yanga. TFF ilimpa Mkwasa nafasi ya kuwa kocha wa muda wa Stars baada ya kumfuta kazi Mart Nooij Julai mwaka huu.


Mkwasa pia ni kocha msaidizi wa Yanga. Katika kuiongoza Stars Mkwasa anasaidiwa na Hemed Morocco wa Zanzibar huku Abdallah Kibadeni akiwa mshauri wa ufundi. Habari za uhakika zilizopatikana jana kutoka TFF zilisema Shirikisho hilo limemtaka Mkwasa kufanya maamuzi kwani hakuna kocha anayeweza kufundisha klabu na timu ya taifa kwa wakati mmoja.

"Maamuzi yameshafanywa kwamba Mkwasa inabidi aamue, kubaki Stars au Yanga, atapelekewa taarifa rasmi," alisema mtoa habari wetu. Habari zaidi zinasema, suala la Mkwasa kuendelea kufundisha Yanga ndio sababu ya mkataba wake kuchelewa.

"Mwanzo kamati ya utendaji ya TFF iliamua kumpa mkataba wa muda mrefu, lakini suala likaja kwa mwajiri wake Yanga itakuwaje, mpango huo ukasitishwa, sasa anatakiwa kufanya uamuzi," alisema mtoa habari wetu.Uamuzi huo wa TFF umekuja siku moja baada ya baadhi ya wadau wa soka kuhoji kocha huyo kuendelea kupiga deiwaka Stars huku akiwa mwajiriwa wa Yanga. Miongoni mwa waliohoji suala hilo ni Ofisa Habari wa Simba, Haji Manara ambaye amemwandikia barua ya wazi Rais wa TFF Jamal Malinzi na kuisambaza kwenye blog mbalimbali na mitandao ya kijamii.
 

"Yanga ndiyo yenye mkataba na 'master' (Mkwasa) vipi mtu mwenye mkataba naye kila uchwao yupo na timu ya taifa? Haki ipi hapa yanga wanaipata?… Lakini mh rais huyo kocha anaweza kujigawa vipi wakati Ligi Kuu inaendelea? je akae kwenye benchi la ufundi la Yanga au akaangalie wachezaji wa timu nyingine?… "Nimetafiti vya kutosha kwenye hili, kocha Boniface (Mkwasa) hajawahi kuhudhuria mechi yoyote ya Simba baada ya kuteuliwa kuwa kocha wa timu ya taifa zaidi ya mechi baina ya Simba na Yanga ambayo yeye ni kocha msaidizi, simaanishi kuwa hapendi kuangalia Simba ila muingiliano wa majukumu unambana…
 

"Na kwa hili nina hakika mechi nyingi za Ligi Kuu za timu nyingine kocha Mkwasa ameshindwa kuhudhuria na kuona wachezaji wengine zaidi ya mechi zinazohusisha timu yake," aliandika Manara kwenye sehemu ya barua yake ya wazi kwa Rais Malinzi.

Mkwasa ambaye kwa sasa yupo na Stars kwa maandalizi ya mechi ya kufuzu michuano ya kombe la dunia dhidi ya Malawi katikati ya wiki ijayo, hakuwa tayari kulizungumzia hilo akisema hajapata taarifa rasmi na kwamba atafanya maamuzi baada ya kuzipata. "Sijapata taarifa kutoka TFF kwa hiyo siwezi kuzungumzia hilo, nitakapopata taarifa, nitajua nini nifanye na nitatoa maamuzi," alisema. Hata hivyo habari za uhakika kutoka kwa watu wa karibu na Mkwasa zinasema kocha huyo yupo tayari kuachia Yanga na kubaki na Stars kwa vile kuwa na kazi mbili kwa wakati mmoja kunamchosha.
 

"Mwenyewe anasema anachoka kuhudumia timu zote mbili, nadhani ataondoka Yanga na kubaki Stars kwa kuzingatia uzalendo pia na mapenzi kwa nchi yake," alisema. Mwisho.

Chanzo: Habari leo
Previous
Next Post »
Show Comments: OR

Contact us

Name

Email *

Message *

Tangaza nasi

Tangaza nasi
Freebango.com